Rais wa Marekani, Donald Trump ametangaza usitishwaji wa mchango wa Marekani kwa Shirika la Afya Duniani (WHO) utaanza kutekelezwa mara moja ndani ya siku thelathini, ikiwa shirika hilo halitafanya maboresho makubwa ambayo aliyapendekeza.
Rais Trump mara kadhaa amekuwa akilishutumu Shirika la Afya Duniani kwa kuruhusu ugonjwa wa COVID -19 kushindwa kudhibitika na kupuuzia athari za ugonjwa huo, ambao umesababisha vifo vya maelfu ya watu duniani.
Mlipuko wa Corona tayari umesababisha vifo vya zaidi ya watu 316,000 ulimwenguni, na Marekani ndio nchi iliyoathiriwa zaidi ambapo imeripotiwa kuwa vifo zaidi ya watu 90,000 na karibu watu milioni 1.5 wameambukizwa virusi vya Corona.
Rais Trump ambaye ameendelea kukosoa Shirika hilo kwa usimamizi wake dhidi ya janga hili, ametoa mwezi mmoja kwa WHO kupata matokeo muhimu.
Katika ukurasa wake wa Twitter Trump aliandika hivi; "Iwapo WHO haitafanya maboresho makubwa ndani ya siku 30, nitabadilisha uamuzi wa awali wa kusitisha kwa muda mchango wa fedha wa Marekani kwa shirika hilo na kuchukua hatua muhimu ikiwa ni pamoja na kusitisha uanachama wetu kwa Shirika la Afya Duniani".
Rais wa Marekani Donald Trump , ambaye anakabiliwa na uchaguzi mkuu mwaka huu ambaye amekosolewa jinsi anavyotatua ugonjwa huo nchini Marekani, Na pia amesikika mara nyingi akilaumu nchi ya China juu ya ugonjwa huo, na wakati huohuo amekuwa akiilaumu WHO kwa kushindwa kuiwajibisha China.