Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema amethibitisha kutokea kwa vurugu za wagonjwa waliowekwa katika uangalizi ambao walikutwa na maambukizi ya corona katika Hospitali ya Amana wakitaka kutoroka hospitalini hapo na kurejea nyumbani.
Leo asubuhi katika mitandao ya kijamii, ilisambaa sauti ikielezea wagonjwa katika Hospitali ya Amana wenye maambukizi ya virusi vya corona kutoroka na wengine kupanda daladala hali iliyozua hofu katika jamii.
Wagonjwa hao wanadaiwa kutoroka hospitalini hapo leo Alhamisi Aprili 23, wakidai kuna msongamano wa wagonjwa wengi huku kukiwa hakuna dawa wala chakula na wao wanaendelea vizuri lakini hawaruhusiwi kurejea nyumbani.
Akitoa ufafanuzi wakati akihojiwa na Kituo cha Televisheni cha ITV, Bi. Mjema amesema si kwamba wametoroka ila wagonjwa hao wamechoka kukaa ndani ya kituo hicho cha uangalizi na hawataki kuendelea kukaa hospitalini hapo.
Bi Mjema amesema kuwa;“Kuna wagonjwa walikuwa wamefika pale wakasema wao hawaumwi sana kwa hiyo walikuwa wanataka waruhusiwe, sasa ukifika pale kama una dalili za maambukizi ya corona lazima ukae kwanza uangaliwe, sasa wao hawataki wanataka waruhusiwe walikuwa wanapiga kelele wanataka kuondoka".
Amesema kuwa endapo mtu ana viashiria au dalili za corona, na ana wasiwasi wa kujiona si mzima, anapaswa kuchukua tahadhari haraka na amewashauri watu kuacha kuamini mambo yanayosemekana mtaani bali wasikilize serikali pamoja na wataalamu wa afya wanachosema, Pia waache kufanya vurugu kwani kufanya hivyo haisaidii kumaliza janga hili la ugonjwa wa Corona.