Wizara ya afya nchini Rwanda imesema kuwa watu wengine wawili wamepatikana na virusi vya corona na kuongeza idadi ya wagonjwa kufikia kuwa na visa saba vya homa ya corona, idadi ambayo ni kubwa zaidi kuliko iliyotangazwa katika mataifa ya jirani ya Afrika Mashariki.
Wizara ya afya nchini humo imesema kuwa watu walioambukizwa coronavirus ni: Mwanamke mmoja Mnyarwanda aliyeolewa na Mnyarwanda mwenzake ambaye aligua baada ya kutembea katika nchi za Fiji, Marekani na Qatar''
Mwingine ni Mjerumani mwenye umri wa miaka 61 aliyewasili Rwanda tarehe 13/03 akitokea Ujerumani kupitia Uturuki, ambaye alifika Rwanda akiwa na kikohozi na kupelekwa hospitalini Machi 15.
Wizara hiyo imesema inawatafuta watu wanaoamini kuwa huenda walichangamana na watu hao ili wapimwe na kufahamu kama wana maambukizi ya ugonjwa huo.
Serikali ya Rwanda ilitangaza kuchukua hatua kadhaa za dharura kukabiliana na janga la coronavirus, saa kadhaa baada ya kutangaza kwamba raia mmoja wa India aliyewasili nchini humo Machi 8, kuthibitishwa kuwa na virusi vya corona.
Katika mahojiano na Radio Rwanda, Mawaziri Anastase Shyaka wa mambo ya ndani na Dr Ngamije Daniel wa Afya, walisema kuwa hatua hizo ni pamoja na kufungwa kwa shule zote za umma na za kibinafsi, maeneo ya kuabudu na sehemu zote za umma.
Bwana Shyaka alisema pia kwamba makasisi wanaelewa ukubwa wa janga hili ambalo Rwanda na dunia nzima inakabiliana nalo.
Miongoni mwa hatua hizo, Bwana Shyaka alisema kwamba matukio kama vile mikusanyiko ya watu katika maeneo ya michezo na harusini ambayo yameahirishwa na kwamba wale waliopoteza wapendwa wao watazikwa kwa namna ya kipekee.
Wizara ya afya inasema muda wa kufunga shule na makanisa wa wiki mbili uliotangazwa unaweza kuongezwa zaidi kutokana na kasi ya maambukizi ya coronavirus nchini humo.
Mwisho.