Daktari wa China ambaye alikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kutoa taarifa kuhusu mlipuko mpya wa virusi vya Corona amefariki dunia kutokana na maambukizi ya virusi hivyo mapema siku ya leo Ijumaa Februari 07, 2020.
Taarifa za kifo cha daktari huyo anayejulikana kwa jina la Li Wenliang zimetengazwa na hospitali yake aliyokuwa akifanyia kazi.
Li Wenliang ambaye alikuwa daktari wa magonjwa ya macho amefariki kutokana na maambukizi hayo alfajiri ya leo Februari 07 ambapo hospitali kuu ya Wuhan imesema katika taarifa iliyochapishwa kwenye akaunti yake rasmi kwenye jukwaa la mtandao wa kijamii nchini China ya Weibo juu ya kifo cha daktari huyo ni za kweli.
Kufuatia hatua hiyo, serikali ya China imetangaza kuanzisha uchunguzi maalum kuhusu kifo cha daktari huyo ambaye ripoti zinasema kuwa, alitishwa alipojaribu kuzungumzia maambukizi hayo hatari ya virusi hivyo vya corona.
Kufikia siku ya leo Ijumaa tayari watu 630 wamepoteza maisha na wengine 31,000 wameambukizwa ugonjwa huko nchini China.
Rais wa China Xi Jinping na mwenzake wa Marekani Donald Trump ambao wamekuwa wakitofautiana kibiashara, wamezungumzia kuhusu maambukizi ya Corona.
Aidha, Beijing imekasirishwa na hatua ya Marekani kuwazuia watu waliotoka nchini China hivi karibuni kutembelea nchi ya Marekani.
Mwisho.