Jumla ya watuhumiwa sita wa mauaji ya aliyekuwa mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Katoro ya Islamic seminari kwa kumtuhumu kujihusisha na mapenzi ya jinsia moja Mudy Muswadiku aliyekuwa na umri wa miaka kumi na tisa wamefikishwa katika mahakama ya wilaya ya Bukoba mkoani Kagera kwa mara ya kwanza. Watuhumiwa hao ni mlinzi wa shule ya sekondari ya Katoro ya Islamic Seminari Badru Tibagililwabe, Majaliwa Abdul ambaye ni mwalimu shuleni hapo, pamoja na wanafunzi wanne ambao wanashtakiwa kwa tuhuma za kumpiga na kisha kumsababishia kifo cha Mudy Muswadiku mwanafunzi wa kidato cha nne mnamo tarehe 4 Aprili mwaka huu. Watuhumiwa hao wamefikishwa mbele ya hakimu mkazi wa mahakama ya wilaya ya Bukoba Frola Kaijage na kusomewa kesi ya mauaji namba 18 ya mwaka 2019 na kaimu mkuu wa mashtaka mkoa wa Kagera wakili Chema Maswi ambaye aliiambia mahakama hiyo kuwa upelelezi bado unaendelea.
Hakimu mkazi Frola Kaijage amewataka watuhumiwa hao kutojibu chochote kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na uwezo wa kusikiliza kesi hiyo. Kesi hiyo imehairishwa hadi Septemba kumi na sita mwaka huu.