Mwanaharakati mwenye asili ya Jamhuri wa Kidemokrasia ya Congo ametozwa faini ya Euro 1000 kwa kuondoa sanamu ya Afrika kutoka makumbusho moja ya Paris.
Mwanaharakati huyo anadaiwa kutenda kosa hilo katika maandamano ya kupinga wizi wa sanaa za Afrika kulikotekelezwa enzi ya ukoloni yanayolenga Ufaransa.
Emery Mwazulu Diyabanza alichukua sanamu ya mbao ya karne ya 19 kutoka makumbusho ya Quai Branly mnamo mwezi Juni katika maandamano yaliyooneshwa moja kwa moja kwa njia ya mtandao.
Diyabanza Alisema; "Nimekuja kuchukua kilichoibwa Afrika".
Jaji aliyekuwa akimtoza faini kubwa ya wizi Diyabanza, hakimu alisema anataka kumaliza tabia za aina hiyo; "Kuna njia zingine unazoweza kutumia kuvutia wanasiasa na umma, kuhusu suala la wizi wa vitu vya kale vilivyochukuliwa wakati wa ukoloni"- Jaji alisema.
Wanaharakati wengine watatu walioungana na Diyabanza katika makumbusho walipigwa faini ya euro 250, 750, na 1,000, kila mmoja, kulingana na shirika la habari la AFP huku wa nne alifutiwa mashtaka.
Katika video ya nusu saa iliyowekwa kwenye mtandao wa Youtube, Diyabanza anaonekana akichukua kinyago kutoka sehemu ilipowekwa.
Yeye pamoja na wanaharakati wengine wakaibeba huku wakipaza sauti na kusema "tunaipeleka nyumbani" lakini wanazuiwa na walinzi kuondoka kwenye makumbusho hiyo.
Diyabanza, kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, amekuwa akishiriki maandamano ya aina hiyo katika miji mingine ya Ufaransa na Uholanzi.
Mwezi uliopita aliliambia gazeti la New York Times: "Ukweli ni kwamba nahitajika kulipa pesa yangu kuona kile kilichochukuliwa kwa nguvu, urithi huu ambao ni wa nyumbani ninakotoka - hapo ndio nilifikia uamuzi wa kuchukua hatua."
Sanamu aliyochukua Diyabanza inasemekana kwamba ilikuwa ni zawadi kutoka kwa daktari wa Ufaransa.
Chanzo: bbc Swahili.